Singida FG yaingia kambini kuiwinda Yanga

© Kwa Hisani

KANDANDA Singida FG yaingia kambini kuiwinda Yanga

Zahoro Mlanzi • 22:00 - 23.10.2023

Singida FG wanajiandaa na mechi hiyo huku wakiwa na kumbukumbu nzuri ya ushindi wa 3-2 kwenye mchezo wao uliopita waliocheza ugenini dhidi ya Namungo.

Kikosi cha timu ya Singida FG, kimewasili na kukita kambi jijini Dar es Saalam tayari kujiandaa kuikabili Yanga kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara unaotarajiwa kupigwa Ijumaa Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Singida FG wanajiandaa na mechi hiyo huku wakiwa na kumbukumbu nzuri ya ushindi wa 3-2 kwenye mchezo wao uliopita waliocheza ugenini dhidi ya Namungo.

Wakiwa chini ya Kocha wao mpya, Ricardo Ferreira raia wa Brazil, Singida FG wanatarajia kuutumia Uwanja wa Uhuru katika maandalizi yao kuelekea mchezo huo.

Akizungumza na Pulse Sports mara baada ya kuwasili Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Singida FG, Hussein Masanza, amesema wachezaji wao wote ni wazima wa afya na kwamba wapo tayari kwa ajili ya kupokea maelekezo kutoka benchi la ufundi.

"Tunashukuru Mungu mechi ya Namungo imeisha salama tumevuna alama tatu, kwasasa baada ya kufika Dar es Salaam tunatarajia kuanza maandalizi yetu haraka iwezekanavyo ili kuwakabili Yanga kwenye mechi yetu inayokuja," amesema.

Baada ya kupata ushindi dhidi ya Namungo kikosi cha Singida kimejisogeza hadi nafasi ya saba wakiwa na alama 8 baada ya kushuka dimbani mara sita.

Katika mchezo uliopita, mabao yao yalifungwa na viungo Mkenya, Duke Abuya dakika ya 45 na Mtogo, Marouf Tchakei mawili dakika ya 68 na 81.