Kocha Azam afunguka kutolewa Mapinduzi Cup

KANDANDA Kocha Azam afunguka kutolewa Mapinduzi Cup

Zahoro Mlanzi • 16:32 - 09.01.2024

Timu hiyo ni msimu wake wa pili mfululizo inatolewa na Singida Fountain Gate katika michuano hiyo.

Kocha wa timu ya Azam FC, Yusuph Dabo, amesema walihitaji kufanya vizuri zaidi katika michuano ya Mapinduzi Cup mwaka huu.

Dado ameyasema hayo mara baada ya kupokea kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Singida FG katika mchezo wa robo fainali.

Akizungumza katika mkutano wake na waandishi wa habari, Dabo amesema walipanga kuitumia michuano hiyo kwa ajili ya kujiimarisha zaidi kwenye kikosi chao na hivyo walitarajia kufika hadi hatua ya mwisho.

"Hatukuwa na dhamira ya kutoka katika hatua hii, tulifanya maandalizi yakutufanya kuendelea kuwa ndani ya mashindano kwa muda mrefu zaidi," amesema.

Katika mchezo dhidi ya Singida FG, timu ya Azam ilikuwa ya kwanza kufunga bao kipindi cha kwanza kupitia kwa Allasane Diao. Hata hivyo Singida FG ilisawazisha bao hilo kipindi cha pili kupitia kwa Mkenya, Elvis Rupia na Habib Kyombo.

Azam ndio mabingwa mara nyingi zaidi wa michuano hiyo wakiwa na rekodi ya kuchukuwa taji hilo mara tano.

Hata hivyo, kwa mara ya pili mfululizo wamekuwa wakikwama kuvuka kisiki cha Singida FG. Msimu uliopita timu hizo zilikutana katika hatua ya nusu fainali ambapo Singida waliwafunga Azam kwa mabao 4-1.