Al Ahly yatua Dar kuivaa Yanga SC michuano ya Afrika

KANDANDA Al Ahly yatua Dar kuivaa Yanga SC michuano ya Afrika

Zahoro Mlanzi • 09:11 - 01.12.2023

Ni kwa ajili ya mchezo wa hatua ya makundi wa Ligi ya Mabingwa Afrika, utakaopigwa Jumamosi.

Mabingwa wa Afrika, timu ya Al Ahly, imewasili jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo kwa ajili ya kuumana na Yanga SC katika mchezo wa hatua ya makundi Ligi ya Mabingwa Afrika.

Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa Jumamosi kuanzia saa 1 usiku kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Al Ahly wamekuja tena Tanzania baada ya kuumana na Simba SC katika robo fainali ya michuano ya AFL iliyoanza Oktoba 20.

Miamba hiyo ya Afrika, iliitoa Simba kwa faida ya mabao ya ugenini baada ya kutoa tena sare ya 1-1 kwenye mchezo wa marudiano Oktoba 24 Uwanja wa Kimataifa wa Cairo jijini Cairo nchini Misri, huku awali ikitoka sare 2-2.

Timu hiyo imetua Dar es Salaam ikiwa imetoka kushinda mechi ya kwanza ya Kundi D mabao 3-1 dhidi ya Medeama FC ya Ghana huku Yanga ikichapwa 3-0 ugenini dhidi ya CR Belouizdad ya Algeria.

Ahly imetua na nyota wake wote akiwemo Mohamoud Kahraba na Pecy Tau ambaye alikosekana katika mchezo uliopita wa Ligi Kuu ya Misri ikielezwa alikuwa majeruhi.

Kwa upande wa Yanga, imeendelea na maandalizi yao katika viunga vya Avic Town na mchezo huo wameupa heshima kwa kuuita Bacca Day kutokana na kazi nzuri inayofanywa na mlinzi wao, Ibrahim Abdullah ' Bacca'.