Simba SC, Yanga SC zapangwa na 'vibonde' michuano ya ASFC

KANDANDA Simba SC, Yanga SC zapangwa na 'vibonde' michuano ya ASFC

Na Zahoro Mlanzi • 22:00 - 29.11.2023

Michuano hiyo hushirikisha timu za madaraja mbalimbali za soka la Tanzania kuanzia Ligi Kuu hadi Daraja la Tatu ambapo bingwa huiwakilisha nchi katika Kombe la Shirikisho Afrika

Mabingwa watetezi wa michuano ya Kombe la Shirikisho la Azam 'ASFC', timu ya Yanga SC, inatarajia kuanza kampeni ya kulitetea taji lao kwa kuwakaribisha Haulung FC ya Njombe.

Yanga ametwaa taji hilo kwa misimu miwili mfululizo na kama watachukuwa msimu huu basi itakuwa ni rekodi kwa kushinda mara tatu mfululizo kitu ambacho hakijawahi kutokea tangu kuanza kwa michuano hiyo.

Mechi za michuano hiyo, itaanza Desemba 15 hadi 17 ambapo timu 64 ikiwemo za Ligi Kuu na zile za madaraja ya chini zote zitatafuta nafasi ya kwenda 32 Bora.

Kwa mujibu wa droo iliyochezwa jijini Dar es Salaam, wana fainali ya michuano hiyo kwa msimu uliopita, Azam FC wataanzia nyumbani kuumana na Alliance FC huku Simba SC wao wakiwaalika Tembo FC.

Timu ya Singida Fountain Gate ambao msimu uliopita walifika hatua ya nusu fainali na kutolewa na Yanga, safari hii wamepangiwa kuanza na Arusha City na mchezo huu utapigwa kwenye Uwanja wa Liti mkoani Singida.

Katika hatua hiyo, timu zote 16 zinazoshiriki ligi kuu bara zimepangwa kuanzia nyumbani.

Timu zitacheza mechi za mtoano ambapo mshindi atapatikana ndani ya dakika 90 na kama mechi ikiisha kwa sare basi mshindi atapatikana kwa mikwaju ya penalti.

Mtindo huo utatumika hadi kwenye hatua ya robo fainali na kwenye hatua ya nusu fainali kutakuwa na dakika 30 za nyongeza.

Kumbuka kuwa bingwa wa michuano hiyo anapata nafasi ya kuwakilisha nchi katika michuano ya Shirikisho barani Afrika.

Tags: