Yanga SC yaanza matizi Avic Town

Wachezaji wa Yanga SC, Maxi Nzengeli (kulia), akiwa na Khalid Aucho wakati wa mazoezi

KANDANDA Yanga SC yaanza matizi Avic Town

Na Zahoro Juma • 16:03 - 17.01.2024

Timu hiyo imeanza mazoezi kujiandaa na mashindano mbalimbali baada ya kutoa mapumziko ya siku 10 kwa wachezaji wake

Kikosi cha timu ya Yanga SC, kikiwa na nyota wake wote, akiwemo mchezaji wao mpya raia wa Ghana, Augustine Okrah, kimerejea mazoezini tayari kujiandaa na michezo yao inayofuata.

Mara baada ya timu hiyo kuondolewa kwenye michuano ya Mapinduzi Cup katika hatua ya robo fainali, Kocha Miguel Gamondi, alitoa mapumziko ya siku 10 ambayo sasa yameisha na timu hiyo imerejea kwenye maandalizi yao ya kumalizia msimu.

Wachezaji ambao wameonekana mazoezini ni wale wote ambao hawapo na timu zao za taifa kwenye michuano ya Afcon nchini Ivory Coast.

Baadhi ya nyota ambao walihusika na mazoezi ambayo yanayoendelea Avic Town, mjini Kigamboni ni pamoja na Pacome Zouzoua, Khalid Aucho, Kouassi Yao ambao hawakushiriki na wenzao katika michuano ya Mapinduzi Cup visiwani Zanzibar.

Kwenye mazoezi hayo, pia alikwemo Okrah ambaye alitambulishwa Zanzibar wakati wa michuano ya Mapinduzi Cup na alipata nafasi ya kuanza katika mchezo dhidi ya KVZ ambapo alidumu uwanjani kwa dakika 16 kabla ya kuumia.

Hata hivyo, mshambuliaji mpya wa Yanga raia wa Ivory Coast, Joseph Guede ambaye alitambulishwa siku ya mwisho wa usajili bado hajawasili nchini na anatarajiwa kujiunga na wenzake muda wowote kuanzia sasa.

Yanga inakabiliwa na kibarua cha kulitetea taji lao la Ligi Kuu Bara msimu huu wakiwa nyuma ya Azam ambao wanaongoza ligi kwa alama 30 hadi ligi iliposimama.

Pia katika michuano ya kimataifa, Yanga wamebakisha mechi mbili za hatua ya makundi Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo bado wana nafasi ya kutinga robo fainali kama watafanya vizuri kwenye mechi hizo.

Kwa mujibu wa Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga, Ali Kamwe, amesema wakati timu hiyo inaendelea na maandalizi pia watacheza mechi za kirafiki za ndani ili kuweka miili sawa.