Wachezaji 21 Tembo Warriors waingia kambini michuano ya Afrika

KANDANDA Wachezaji 21 Tembo Warriors waingia kambini michuano ya Afrika

Zahoro Juma • 10:00 - 23.01.2024

Hiyo ni timu ya Soka ya Taifa ya Tanzania ya watu wenye ulemavu ambayo inajiandaa na michezo ya AFCON kwa Walemavu

Wachezaji 21 wameitwa kwenye timu ya Taifa ya watu wenye Ulemavu 'Tembo warriors’, itakayojiandaa kushiriki mashindano ya Afrika yatakayofanyika Aprili 14 hadi 29 mwaka huu, nchini Misri

Tanzania ilimaliza nafasi ya nne katika mashindano kama hayo na kufanikiwa kupata nafasi ya kufuzu kushiriki Kombe la Dunia ambalo waliishia hatua ya robo fainali.

Akitangaza kikosi hicho Dar es Salaam, Kocha Mkuu wa timu hiyo, Salvatory Edward, ametaja wachezaji watakaoingia kambini ni Bashara Alombile, Ally Juma Abdallah, Hassan Vuai Ameri, Abdulkarim Amin Khalifa, Shadrack Hebron Sembele, Richard Fredy Swai, Ramadhan Ally Chomero.

Wengine ni Juma Mohamed Kidevu, Salimu Rashid Bakari, Steven Manumba Antony, Habibu Saidi, Salehe Mwipi, Khalfan Athumani, Emmanuel Nakala, Adamu Hassan, Lifati Anasi, Rojas Kadora, Julius Ngume, Kassimu Mohamed, Frank Ngairo na Wistin Sango.

Kwa upande wea Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Mpira wa Miguu kwa watu wenye Ulemavu Tanzania (TAFF), Athumani Lubandame, amesema timu imeanza kambi ya kwenda na kurudi kwa ajili ya mandalizi ya mashindano hayo.

Amesema kambi hiyo itafanyika kwa mwezi mmoja na baadaye kuingia kambi ya pamoja.

"Sasa timu imeanza mazoezi rasmi leo (Jana) ambayo yanafanyika Uwanja wa Uhuru kwa mwezi mmoja na tukiwa tunasubiri maelekezo ya serikali kuingia kambi ya pamoja baadaye," amesema Lubandame.

Kwa upande wa Meneja wa timu hiyo, Zaharani Mwenyemti, amesema wanataka kufika fainali katika mashindano hayo.

Tags: