Singida FG kukaa kambi ya siku 10 Mwanza

Kocha Frank Peterson (katikati), akishukuru baada ya makubaliano hayo

KANDANDA Singida FG kukaa kambi ya siku 10 Mwanza

Zahoro Juma • 22:00 - 30.01.2024

Lakini pia klabu hiyo imeingia ushirikiano na Kocha, Mdenmark Frank Peterson ili aibue vipaji na kuvitafutia masoko nje ya nchi

Kikosi cha timu ya Singida FG, kimetua mkoani Mwanza, tayari kujiandaa kwa ajili ya kukabiliana na mechi tatu mfululizo za michuano ya Ligi Kuu Bara ambazo zote watacheza ugenini.

Kutokana na ratiba hiyo, uongozi wa timu hiyo uliamua kuweka kambi ya muda mkoani humo ikiwa kama sehemu ya maandalizi ya kufanya vizuri katika mechi zote tatu.

Singida FG itashuka uwanjani Februari 12 kuumana na Uwanja wa Kaitaba kucheza na wenyeji wao Kagera Sugar.

Mara baada ya mchezo huo ambao utakuwa ni wa kumalizia mzunguko wa kwanza, Singida FG watalazimika kusafiri hadi Mbeya ili kucheza na Tanzania Prison, Februari 15.

Mchezo wa mwisho wa ugenini kwa Singida FG katika ratiba hiyo utakuwa ni dhidi ya Tabora United ambao umepangwa kuchezwa Februari 25.

Akizungumza kwa simu na Pulsesports akiwa jijini Mwanza, Ofisa Habari wa Singida FG, Hussein Masanza, amesema wameamua kuweka kambi hiyo ya Kanda ya Ziwa mapema ikiwa ni sehemu ya maandalizi yao.

Amesema benchi la ufundi walipendekeza kambi ya aina hiyo kwa ajili ya kupata utulivu na muda mwingi wakiwa na wachezaji wote wa kikosi cha kwanza.

Hamu kubwa ya mashabiki wa soka wa Tanzania wanatamani kuona ni namna gani Singida FG itarejea kwenye ligi hiyo hasa baada ya kuondokewa na nyota wake wengi katika usajili wa dirisha dogo uliofungwa mapema mwezi huu.

Wachezaji ambao waliondoka kikosini hapo ni pamoja na Elvis Rupia, Marouf Tchakei, Duke Abuya, Gadiel Michael, Meddie Kagere na Mourice Chukwu.

Katika hatua nyingine, Klabu hiyo, imeingia ushirikiano na Kocha wa kimataifa wa Denmark, Frank Peterson, kuwaongezea thamani wachezajia wazawa na kuwasaidia kupata nafasi kucheza nje ya Tanzania.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na klabu hiyo kupitia mitandao yao ya kijamii, Peterson atashirikiana na klabu hiyo katika eneo la kuibua vipaji na kuvitafutia fursa nje ya nchi.

"Ushirikiano huu utahusu timu zetu za vijana, wanaake na timu ya wanaume," imeeleza taarifa ya timu hiyo.