Sababu 3 Taifa Stars kufungwa na Morocco

KANDANDA Sababu 3 Taifa Stars kufungwa na Morocco

Zahoro Mlanzi • 14:07 - 22.11.2023

Katika mchezo huo, Stars imemaliza pungufu baada ya nyota wake, Novatus Dismas kuoneshwa kadi ya pili ya njano

Timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars', imepoteza mchezo wake wa kwanza katika harakati za kufuzu Kombe la Dunia 2026 kwa kufungwa mabao 2-0 nyumbani na Morocco.

Mchezo huo umepigwa Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam ambapo Morocco walifunga mabao ya kupitia kwa Hakim Ziyech na lingine likiwa ni la kujifunga kupitia Lusajo Mwaikenda.

Katika mchezo huo, Stars ilimaliza pungufu baada ya nyota wake, Novatus Dismas kuoneshwa kadi ya pili ya njano kwa kushikana mashati na Ziyech ambaye pia alioneshwa kadi ya njano.

Hata hivyo baada ya mchezo huo kiungo huyo ambaye kwasasa anacheza Ligi ya Ukraine akiwa na Shakhtar Donetsk, ameomba radhi kupitia mtandao wake wa kijamii wa Instagram.

Kabla ya kufungwa kwa mabao hayo, dakika za awali beki wa kulia wa Morocco anayecheza kwenye Klabu ya PSG ya Ufaransa, Achraf Hakimi, alipoteza mkwaju wa penalti ambalo mpira wake uliota mbawa.

Baada ya mchezo huo kumalizika, msimamo sasa unaonesha kuwa Morocco ndio vinara wa Kundi E wakiwa na alama tatu sawa na Zambia, Niger na Taifa Stars ila zinatofautiana kwa mabao.

Timu ya Congo Brazaville wao wapo nafasi ya tano wakiwa hawana alama yoyote.

Baada ya matokeo hayo, Pulsesports inakuleta sababu tatu ilizofanya Taifa Stars kupoteza mchezo huo.

Ubora wa mpinzani

Kabla ya kuongea au kulaumu chochote lazima kwanza watu wakiri ubora wa wapinzani ambao Stars imecheza nao.

Ikumbukwe Morocco inashika nafasi ya kwanza kwa ubora wa viwango Afrika huku Tanzania ikiwa nafasi ya 31 na katika upande wa dunia Morocco wapo nafasi ya 13 na Tanzania 121.

Hata aina ya wachezaji wao na timu wanazocheza ni kielelezo tosha ya kuonesha ni kwa namna gani wameizidi Stars katika idara nyingi uwanjani.

Bao la kwanza la mchezo ambalo lilifungwa na Ziyech ni aina ya mabao ambayo amekuwa akifunga hata kwenye ligi mbalimbali za ulaya ambazo amekuwa akicheza kwa miaka kadhaa.

Upangaji wa kikosi

Ni wazi huenda mlinda lango wa Stars, Kwesi Kawawa angeweza kufanya vizuri zaidi ya alivyofanya pale lakini kama lawama watapewa makipa wengi kwa aina ile ya mabao ya Ziyech.

Hata hivyo licha ya kuwa Morocco wapo juu kisoka na kila kitu lakini Stars pengine ingeweza kufanya jambo kama walau Kocha, Adel Amrouche angepanga kikosi chetu katika hali ambayo inaridhisha.

Kulikuwa na nafasi ndogo ya kuwafunga au kufanya vizuri dhidi ya Morocco lakini hata hiyo nafasi haikutumika vizuri kwa kupanga kikosi ambacho hakikuwa na ushawishi uwanjani.

Wachezaji wote ni watanzania lakini nyota Mbwana Samatta, Simon Msuva, Aishi Manula na hata Feisal Salum 'Fei Toto' pengine wangeweza kufanya kitu zaidi ya ambacho kimefanyika kutokana na uzoefu wa wachezaji hao kikosini.

Mfumo uliotumika

Kitu kingine kilichoiangusha Stars kwenye mchezo huo ni aina ya mfumo ambao ameutumia Kocha Amrouche.

Kocha huyo aliamua kuwaheshimu zaidi wapinzani kitu ambacho sio kibaya lakini alikosa mipango wakati Stars ikiwa na mpira.

Hiyo ilitokana na wachezaji waliokuwepo uwanjani kwa ajili ya kutengeneza mfumo huo. Viungo wa kati, Himid Mao na Sospter Bajana hawana uwezo mkubwa wa kuchezesha timu hasa mpira unapokuwa katika himaya ya Stars na hilo lilionekana katika mchezo.

Matokeo yake mshambuliaji pekee aliyekuwepo ambaye ni Kibu Denis akawa anakosa huduma ya mipira mizuri na hiyo iliwafanya walinzi wa Morocco, Roman Saiss na Nayef Aguerd wacheze kwa uhuru mkubwa.