Novatus awa Mtanzania wa tatu kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya

© Kwa Hisani

KANDANDA Novatus awa Mtanzania wa tatu kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya

Zahoro Mlanzi • 12:09 - 20.09.2023

Novatus kabla ya kusajiliwa na Donetsk katika dirisha la usajili lililopita msimu huu, alikuwa akiichezea Zulte Waregem ya Ubelgiji.

Kiungo Mtanzania, Novatus Dismas, ameingia kwenye orodha ya wachezaji waliowahi kucheza michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, baada ya kuichezea timu yake ya Shakhtar Donetsk dhidi ya FC Porto usiku wa kuamkia leo.

Wachezaji wengine wa Kitanzania waliowahi kucheza mashindano hayo ni Kassim Manara akiwa na Admira ya Austria na Mbwana Samatta akiwa na Genk ya Ubelgiji.

Katika mchezo huo wa kwanza wa Kundi H hatua ya makundi, hadi kipindi cha kwanza kinamalizika, Shakhtar walikuwa nyuma kwa mabao 3-1 uwanjani Volksparkstadion jijini Hamburg, Ujerumani.

Mabao ya FC Porto yamefungwa na mshambuliaji wake Mbrazil, Wenderson Galeno akipachika mawili dakika ya nane na 15 na Muiran Mehdi Taremi dakika ya 29.

Bao pekee la Donetsk limefungwa na Kevin Kelsy dakika ya 13 ambapo imelazimika kuchezea mechi zake za nyumbani nchini Ujerumani kutokana na machafuko yanayoendelea nchini kwao kutokana na uvamizi wa majeshi ya Urusi.

Baada ya mchezo huo kumalizika, mashabiki na wadau wa soka kutoka maeneo mbalimbali wametoa pongezi kwa nyota huyo kutokana na mafanikio hayo.

Mchambuzi wa Michezo nchini Tanzania kutoka Wasafi Redio, Oscar Oscar, amesema Novatus amejiwekea historia binafsi katika soka la kimataifa lakini pia atakuwa ametoa hamasa kubwa kwa vijana wanaokuja kufuata nyayo zake.

Novatus kabla ya kusajiliwa na Donetsk katika dirisha la usajili lililopita msimu huu, alikuwa akiichezea Zulte Waregem ya Ubelgiji.

Baada ya kuibukia katika akademi ya Azam FC, Novatus amecheza pia Biashara United katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara kabla ya kwenda Israel mwaka 2021 ambako alichezea timu za vijana za Maccabi Tel Aviv na Beitar Tel Aviv Bat Yam hadi alipouzwa.