Kocha Ferreira aomba muda Singida FG

© Azam TV

KANDANDA Kocha Ferreira aomba muda Singida FG

Zahoro Mlanzi • 05:31 - 17.10.2023

Ferreira amerithi mikoba iliyoachwa na Mjerumani, Ernst Middendorp pamoja na Mholanzi Hans van Pluijm.

Saa chache baada ya kutangazwa kuwa kocha mpya wa timu ya Singida Fountain Gate, Mbrazil Ricardo Ferreira, ameomba kupewa muda ili aweze kuisuka upya timu hiyo.

Ferreira amerithi mikoba iliyoachwa na Mjerumani, Ernst Middendorp pamoja na Mholanzi Hans van Pluijm.

Akizungumza na Pulsesports, Ferreira amefurahia kujiunga na miamba hiyo na kwamba baada ya kukiona kikosi hicho kwenye baadhi ya mechi amekiri kuwa ni kizuri lakini kitahitaji muda ili kuweza kufika kwenye uwezo mkubwa.

"Nimeona wachezaji wazuri lakini changamoto niliyo nayo ni kwamba msimu unaendelea na sina muda wa kutosha wa maandalizi, hivyo taratibu nitaendelea kuwaelekeza wachezaji wangu ili waweze kujua kitu ambacho ninataka," amesema Ricardo.

Kwa upande wa Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo, Olebile Sikwane, amesema wamefikia makubaliano na kocha huyo baada ya kuvutiwa na rekodi zake za ufundishaji katika timu mbalimbali alizofundisha huko nyuma.

"Tumefikia makubaliano na kocha Ricardo baada ya mchakato wetu wa ndani kukamilika na kuona yeye ni chaguo sahihi kati ya wale ambao tulikuwa tunawachuja," alisema Sikwane.

Ferreira ni kocha ambaye ameacha alama kubwa nchini Sudan kwani aliingia nchini humo mwaka 2005 ambapo alijiunga na Al Hilal na kuisaidia kushinda taji la ligi mara tatu mfululizo huku akiisaidia pia kutinga hatua ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Mbali na Al Hilal kocha huyo pia alifundisha Al Marrekh ya huko huko Sudan kuanzia msimu wa 2021-22 ambapo aliwasaidia kushinda taji la ligi pamoja na kuwapeleka makundi ya Klabu Bingwa Afrika.

Singida FG ambayo imeondolewa kwenye michuano ya Shirikisho Afrika na timu ya Future ya Misri, imecheza mechi tano kwenye Ligi Kuu Bara msimu huu huku ikiwa wameshinda mechi moja, sare mbili na wamepokea vichapo viwili kutoka kwa Simba na Azam.

Kwasasa kocha huyo ana kazi ya kukikonoa kikosi chake kabla ya kukabiliana na mechi mbili za ugenini dhidi ya Namungo na kisha Yanga.